TAIFA STARZ WAFANYIWA UMAFIA ,WATANZANIA WAPAMBANA NA ASKARI


Kocha wa Stars, Kim Poulsen kushoto akipambana na askari wa Uwanja wa Marakech
Na Mahmlud Zubeiry, Marakech, IMEWEKWA JUNI 8, 2013 SAA 8:00 USIKUTIMU ya soka ya taifa ya Tanzania, Taifa Stars usiku huu imekiona cha moto mbele ya askari wa Uwanja wa Marakech, baada ya kufanyiwa vurugu na kuzimiwa taa ishindwe kufanya mazoezi kwenye Uwanja huo siku moja kabla ya mchezo wao na wenyeji wao Morocco kesho, kuwania tiketi ya kucheza Fainali za Kombe la Dunia. Sheria za FIFA zinasema timu mgeni, itapewa fursa ya kufanya mazoezi katika Uwanja utakaotumika kwa mechi dhidi ya wenyeji katika muda ambao mechi itachezwa, lakini leo msafara wa Stars ulipofika Uwanja wa Marakech ulizuiwa kuingia ndani na askari wa uwanjani hapo. Juhudi za Kocha mkuu wa Stars, Kim Poulsen kuwaelewesha askari wa Uwanja huo sheria ili wairuhusu timu kuingia uwanjani hazikuzaa matunda na ikabidi viongozi wa Shirikisho la Soka Tanzania (TFF) waingilie kati, nao pia wakachemsha.
Thomas Ulimwengu kulia nje ya geti, askari kushoto



Dk Dau getini


Mtanzania anaruka geti ili kufungua mlango Stars ikafanye mazoezi


Baadhi ya wachezaji wa Stars, kutoka kulia Juma Kaseja, Amri Kiemba, Mrisho Ngassa na Salum Abubakar baada ya kuingia uwanjani


Kutoka kulia Mwinyi Kazimoto, Athumani Iddi 'Chuji' na Kevin Yondan


Crescentius Magori kushoto akishuhudia marefa wa mchezo huo wakikagua pasipoti za wachezaji wa Stars


Wasiwasi; Kutoka kulia DK Dau, Mh Zitto Kabwe, Mh Mohamed Dewji na Magori wakijadiliana uwanjani

Ikawadia zamu ya viongozi wa Kamati ya Ushindi ya Stars, inayodhaminiwa na Kilimanjaro Premum Lager, ambao nao walichemsha- ndipo baadhi wa Watanzania waishio hapa na wachache waliosafiri kutoka Dar es Salaam walipoongeza nguvu. Walikwenda kufungua geti kwa nguvu, wakawaweka kando askari waliokuwa wanawazuia na kuiingiza timu uwanjani kufanya mazoezi. Hata hivyo, Stars ilipofika uwanjani ililazimika kusubiri tena, kwani wenyeji Simba wa Atlasi walikuwa wakiendelea na mazoezi. Baada ya nusu saa, Morocco walimaliza awamu yao na Stars wakaanza kupasha misuli moto. Hata hivyo, baada ya dakika 34, taa za Uwanja huo zilizimwa na uwanjani kuwa giza totoro, lakini viongozi wa TFF wakaenda kuomba, zikawashwa na timu ikafanya mazoezi kwa dakika 10 zaidi. Naibu Waziri wa Habari Utamaduni na Michezo, Mh. Amos Makalla aliyekuwapo wakati wa vurumai zote hizo, alisikitishwa mno na kitendo hicho akisema si cha kiungwana na si cha kiunamichezo.
Makipa mazoezini; Juma Kaseja amedaka, Ally Mustafa 'Barthez' anamshuhudia kushoto



Shomary Kapombe anayeteleza, Erasto Nyoni akipitisha mpira


Mtanzania amemdhibiti askari wachezaji waingie uwanjani


Wachezaji wakiingia uwanjani kufanya mazoezi


Watanzania wamefanikiwa kufungua geti


Ahmad Mgoyi wa TFF akipambana na askari kufungua geti 


Mpambano, Kim Poulsen na askari, nyuma ni Mgoyi 

Makamu wa Rais wa TFF, Athumani Nyamlani alisema Morocco walikuja kucheza Dar es Salaam walipokewa vizuri na wakahudumiwa vizuri hadi wanaondoka, ajabu leo wanaifanyia ‘unyama’ Tanzania. Mkuu wa Msafara wa Stars hapa, Crescentius John Magori alisema watapeleka malalamiko FIFA, waandaji wa michuano ya kufuzu kwa Kombe la Dunia na kwa kuwa ushahidi upo, anaamini Morocco watachukuliwa hatua. Mwenyekiti wa Kamati ya Usajili ya Simba SC, Zacharia Hans Poppe alishauri Stars icheze chini ya angalizo kwa kuwasilisha barua FIFA mapema ili wakae wanajua kuhusu hali halisi Morocco. Kwa ujumla kilichotokea leo kimewatia woga Watanzania wengi waliopo hapa kuelekea mchezo wa kesho, ambao Stars inahitaji ushindi ili kujiimarisha katika mbio za kuelekea Brazil 2014. Hata ulinzi wa msafara wa Stars kutoka hotelini hadi uwanjani hakuwa wa kutosha na ilishuhuidiwa mara kadhaa ukiingiliwa na magari mengine barabarani wakati timu ikienda uwanjani kwa mazoezi. Wenyeji nchini Morocco wanasema inapowadia mechi, huwa wanaogopa kwa sababu mara nyingi hutokea vurugu ya damu kumwagika. Kwa ujumla Stars inaingia katika mchezo wa kesho katika hali ya wasiwasi na woga mkubwa. Stars itashuka dimbani saa 3:00 usiku kesho kwa saa za hapa sawa na saa 5:00 za Tanzania kucheza na Morocco. Stars inashika nafasi ya pili katika Kundi C, ikiwa na pointi sita nyuma ya Ivory Coast yenye pointi saba, ambayo kesho itakuwa ugenini ikimenyana na Gambia katika mchezo mwingine wa kundi hilo.
Mrisho Ngassa anamiliki mpira



Thomas Ulimwengu anakwenda


Mbwana Samatta kulia na mpira


Wachezaji Stars Uwanja wa Marekch

Stars ilitua hapa Jumatatu ikitokea Ethiopia ambako iliweka kambi ya wiki moja na kucheza mchezo wa kirafiki dhidi ya Sudan, ulioisha kwa sare ya bila mabao.Kabla ya kuja hapa, Stars iliweka kambi ya wiki moja katika hoteli ya Tansoma, Dar es Salaam ikijifua Uwanja wa Karume na siku chache kabla ya kuondoka ilialikwa Ikulu na Rais Jakaya Kikwete, aliyewapa hamasa kwa hotuba nzuri
Credit to bin zubery