MIJI YENYE GHARAMA ZAIDI DUNIA


LONDON, Uingereza
MIJI ya Sydney na Melbourne ni miongoni mwa maeneo yanayotajwa kuwa na gharama kubwa zaidi za maisha duniani.
Miji hiyo ambayo iko nchini Australia, imeingia katika nafasi ya tano bora.
Kwa mujibu wa utafiti uliofanywa na Kitengo cha Kiintelijensia cha Uchumi Duniani (EIU), gharama za maisha katika miji hiyo imezidi hata miji ya Ulaya na Marekani.
Bara la Asia na Australia lina miji 11 kati ya 20 iliyotajwa kuwa na gharama za juu za maisha duniani, huku miji minane ikitoka Ulaya na mmoja ukitoka America ya Kusini.
Kwa mujibu wa taarifa zilizotolewa na kitengo hicho, licha ya bara la Amerika ya Kaskazini kuwa na nchi maarufu na zenye uchumi wa juu, hakuna hata mji mmoja ulioweza kuingia kwenye 20 bora.
Katika utafiti uliofanyika miaka 10 iliyopita kulikuwako na  miji sita kutoka barani Asia, 10 kutoka Ulaya na minne kutoka Marekani katika 20 bora kwenye orodha ya miji 131 yenye gharama za juu kwenye nchi 93 duniani.
Katika utafiti  uliotolewa mwaka huu, Jiji la Tokyo limeshika nafasi ya kwanza likiliweka pembeni Jiji la Zurich ambalo lilikuwa kwenye nafasi hiyo na kuporomoka hadi kufikia nafasi ya saba.
Hii ni kutokana na sera za udhibiti wa mapato ya ndani ya nchi ya Uswiz kushuka.
Mji wa Osaka nchini Japan unashikilia nafasi ya pili katika orodha hiyo.
Jon Copestake, mhariri wa jarida la EIU alisema moja kati ya mabadiliko yaliyojitokeza ilikuwa ni kupanda kwa gharama nchini Australia, kulikouweka Mji wa Sydney kushika nafasi ya tatu huku Melbourne ikishika nafasi ya tano. Mji wa Oslo wa Norway ukishika nafasi ya nne. “Katika kipindi cha miaka kumi iliyopita, miji ya Australia haikuweza kuingia hata kwenye hamsini bora. Sijawahi kuona upandaji huu wa ghafla,” Copestake aliliambia Reuters.
“Lakini hii inatokana na kukua kwa uchumi kunakoendana na mfumuko wa bei pamoja na  kuimarika kwa Dola ya Australia dhidi ya Dola ya Marekani. Wageni wanaofika hapo huona kuna tofauti kubwa ya kimaisha huku wenyeji wakizoea maisha ya juu.
Kupanda kwa gharama barani Asia
Utafiti huo ulifanyika kwa kuangalia gharama za zaidi ya bidhaa 160 ukilenga kwenye vyakula, mavazi, huduma za nyumbani, usafiri na vitu vidogovidogo.
Copestake haikushangaza sana kwa Mji wa Tokyo kurejea kwenye miji ya inayoongoza, hii ni kutokana na kukua kwa uchumi wa Japan jambo linalosababisha kuongezeka kwa gharama za mahitaji muhimu kama vile mapango ya nyumba, mishahara na hata bei za nishati ya mafuta.
Tangu mwaka 1992 Tokyo imekuwa kwenye sita bora huku miji ya  Zurich, Paris na Oslo ikidaiwa kushika nafasi ya kwanza.
Miji mingine iliyoingia kwenye 10 bora kwa mwaka 2013 ni

Singapore, Zurich, Paris,Caracas na Geneva.
Akizungumzia kuhusu nchi za Ulaya, Copestake alisema woga wa kushuka kwa uchumi wao na kuimarika kwa Euro kumechangia kwa kiasi kikubwa kupanda kwa gharama za maisha kwa miji ya bara hilo, huku kwa Mji wa Carcas kumetokana na kukua kwa udhibiti wa viwango vya ubadilishaji wa fedha.
Licha ya kutokuwako kwa miji ya Amerika ya Kaskazini kwenye 20 bora, EIU imesema gharama za maisha kwa mji wa Washington  zilikuwa zikiongezeka ukilinganisha na maeneo mengine ya Marekani. Mji huo umeshika nafasi ya 27 ukifungana na Mji wa Los Angeles.
Mji wa Vancouver wa nchini Canada umeendelea kushika nafasi ya 21, ukiwa ni mji wenye gharama za juu zaidi za maisha kwa nchi za Amerika ya Kaskazini.
Hata hivyo, wakati Bara la Asia na  Australia kuna jumla ya miji 11 iliyoingia kwenye 20 bora, inasemekana ni eneo ambalo lina miji sita kati ya 10 yenye gharama rahisi zaidi duniani.
Mji wa Mumbai kutoka nchini India na Karachi wa Pakistan ni miongoni mwa miji iliyotajwa kuwa na gharama za chini za maisha katika utafiti huo ikifuatiwa na New Delhi, Kathmandu na Algiers.
Nchi ya India imekuwa na tofauti kubwa kimaisha kwa baadhi ya miji kutokana na kuwepo kwa tofauti ya mgawanyo wa miundombinu.
Hii ndiyo sababu kubwa ya kuweko kwa miji yenye gharama za juu zaidi na ile yenye gharama za chini zaidi.
Miji mingine iliyoshika nafasi kumi za mwisho katika utafiti huo ni pamoja na Bucharest wa Romania, Colombo wa Sri Lanka, Panama City, Jeddah wa Saudi Arabia, na Teheran wa Iran.